GARI LA MZEE GURUMO LAZUA UTATA



Mzee Gurumo akikabidhiwa ufunguo wa gari na Diamond.
AMA kweli asiyekuwepo na lake halipo! Lile gari la aliyekuwa mwanamuziki mkongwe wa muziki wa dansi aliyefariki dunia hivi karibuni, Muhidin ‘Maalim’ Gurumo alilopewa na nyota wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond’, limeibua utata mtupu ndani ya familia ya marehemu huyo baada ya kubainika kwamba kumbe hakupewa kadi yake.
Gari aina ya Toyota FunCargo iliyosababisha hali ya sintofahamu kwenye familia ya mzee Gurumo baada ya kufa.
Kwa mujibu wa chanzo makini kutoka ndani ya familia hiyo jambo hilo lilifahamika kufuatia mgogoro mkubwa unaoendelea kufukuta miongoni mwa wanandugu hao ambao sasa wamechangukana kutokana na mgawanyo wa mali za marehemu.
Ilijulikanaje kama hakuna kadi?
Chanzo hicho kilimtaja mtoto wa kike wa marehemu Gurumo aitwaye Mariam ambaye anataka nyumba na gari hilo aina ya Toyota FunCargo viuzwe ili watoto wagawane fedha.

Mke wa marehemu mzee Gurumo Pili Said
“Yule binti alikwenda nyumbani kwa mama yake (mke wa mwisho wa mzee Gurumo aliyekuwa akiishi naye kwenye nyumba yake Mabibo, Dar) na kumtaka ampe kadi ya gari akidai ni la kwake na anataka kuliuza.
“Mama mtu alimwambia mwanaye kuwa baba yao hakupewa kadi hiyo siku alipokabidhiwa gari hilo.

“Hata hivyo, mama huyo alisema siku moja mzee Gurumo alimfuata Diamond alipokuwa akifanya shoo pale Coco Beach (Dar) kwa ajili ya kuulizia kadi hiyo ndipo Diamond akamwambia kwamba akitaka kadi amuulize mtu mmoja aliyesema ni kiongozi mmoja, anafanya kazi maeneo ya Posta Mpya jijini Dar (jina linahifadhiwa kwa sasa),” kilisema chanzo.
Iliendelea kudaiwa kuwa baada ya Gurumo kuambiwa maneno hayo, hakutoa jibu lolote kwa mke wake kama alipewa kadi hiyo au la, lakini mama huyo hakuwahi kuiona.
Kukosekana kwa kadi hiyo kumesababisha kuendelea kuwepo kwa gari hilo, kwani kama ingekuwepo, lingeshauzwa.
Habari kutoka ndani ya kambi ya Diamond zilisema kuwa tukio la kutoa gari kwa mkongwe huyo mwanzilishi wa Bendi za  Mlimani Park Orchestra na Msondo Music Band ulikuwa ni mpango maalum wa kumpromoti msanii huyo ili aweze kung’ara zaidi katika vyombo vya habari ambao uliratibiwa na kiongozi huyo mwenye kulalamikiwa na wasanii mara kwa mara.

Diamond ambaye alipongezwa na wadau mbalimbali kwa kitendo chake hicho kilichoelezwa kuwa cha kiungwana na chenye kupaswa kuigwa, juzi hakupokea simu ya mwandishi alipopigiwa ili kutoa ufafanuzi, kama ambavyo hakujibu ujumbe mfupi (sms) aliyoulizwa kuhusu utata huo.
Hata kiongozi huyo alipopigiwa simu, iliita kwa muda mrefu bila kupokelewa na hata alipotumiwa ujumbe mfupi wa maneno, pia hakujibu.
Mwaka jana Diamond alimpatia mzee Gurumo gari hilo kama sehemu ya kuenzi mchango wake katika muziki wa Tanzania tukio lililofanyika kwenye Hoteli ya Serena, Dar kabla ya mzee huyo kufariki dunia Aprili 13, mwaka huu.

TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

Post a Comment

Ungana Nasi, Like Page Yetu Hapa Chini