UKICHEPUKA MARA MOJA, INAWEZA KUYAGHARIMU MAISHA YAKO YOTE KUREJESHA UPENDO!

Jumanne iliyopita (Aprili 22), niliandika ujumbe katika akaunti zangu za mitandao ya kijamii, Facebook (Luqman Maloto), Twitter (@luqmanmaloto) na instagram (@LuqmanMaloto) wenye lengo la kushauri marafiki zangu kuheshimu mapenzi wanayopata kutoka kwa wenzi wao.
Niliandika: “Kabla hujamfanyia vitimbi mwenzi wako. Kabla hujachepuka, ukamsaliti na kumsababishia maumivu makali ya moyo pamoja na usumbufu usiomithilika katika katika maisha yake, tambua kuwa huyo mwenzi wako hukumuokota jalalani, kwamba alikuwa katupwa, katelekezwa na hakuna mwingine wa kumpenda.

“Kwamba baada ya kutupwa, eti wewe ndiye ukamuokota na kumhifadhi. Tambua kuwa yeye ni mtu kamili, anamezewa mate pia. Ukipuuza utu wake, thamani yake, uzuri wake na mapenzi yake, siku akiondoka utajuta na kuumia kwa kuwaza mazuri yake.
“Akishaondoka, hao uliowaona ni bora hawatakuthamini, watakuchezea kama nyasi za Uwanja wa Taifa. Kwa nini ujute baadaye? Wakati ni huu wa kutimiza wajibu. Mpende akupendaye, usimuumize. Ukithubutu kumuumiza, wewe utajuta zaidi zamu yako ikifika.”
Niliandika ujumbe huo baada ya kuguswa na stori ya msomaji wangu ambaye ni mwanamke. Nilikutana naye Jumanne hiyo saa 5 asubuhi, alinisimulia mkasa wake wa mapenzi, nikamshauri kwa jinsi ambavyo Mungu aliniongoza lakini nikaona si vibaya kuwaandikia marafiki zangu, kama mwenye kasumba ya kumsaliti mwenzi wake au kumfanyia vitimbi, aache.
Siku zote uwe na angalizo kuwa unapomsaliti mara moja lakini akikugundua, inaweza kukugharimu maisha yako yote kubembeleza na kujisafisha ili akupende kama ilivyokuwa mwanzo bila mafanikio.
Kitakachomfanya asirejeshe upendo wa mwanzo ni kumbukumbu za usaliti uliomfanyia na maumivu aliyoyapata.
Wengi hufanya kama utani, wakijua watachepuka mara mbili tatu bila kugundulika. Wakati wa kuanza huo uchepukaji, huwa hawawazi siku ya kunaswa na aibu ambayo wataipata. Utokaji wa njia kuu, imekuwa kama fasheni kwa wanaume na hata wanawake.
Mume ana nyumba ndogo, mke anamiliki kidumu.
Kisaikolojia, ni afadhali kwa asilimia 70 kuachana baada baada ya kufumaniana kuliko kuendelea kwa sababu upendo hauwezi kuwa kama awali.
Imani itashuka kwa kiwango kikubwa. Hata lugha ya mawasiliano hugeuka ya kukoseana adabu baada ya fumanizi.
Tahadhari kuu ndani ya kichwa chako ni kuwa kama unampenda mwenzi wako, usithubutu kufanya jaribio la usaliti hata kwa bahati mbaya. Endapo atakugundua, kuna matokeo mabaya ya aina mbili ambayo utayapata; mosi anaweza kukupiga chini jumla.
Pili ni kuwa endapo atakusamehe, ni vigumu sana kufurahia mapenzi yake kwa sababu imani yake kwako itashuka, kwa hiyo na upendo pia hautakuwa ule wa awali.
Utajisikiaje mtu ambaye alikuwa anakupa mapenzi mazito, baadaye awe anakupimia kwa kukusikilizia kwa sababu hakuamini? Akili ‘kumkichwa’.

HESHIMUPENZILAKE, LINDAPENZILAKO
Unapoingia kwenye uhusiano wa kimapenzi, lengo la juu kabisa la kwako wewe, linatakiwa liwe kumfanya mwenzi wako afurahi kuwa na wewe, vilevile na yeye awe na msukumo unaofanana na huo wa kuhakikisha unafurahia mapenzi yenu siku zote.
Kama kila mmoja ataweka nia hiyo na kuitekeleza kwa vitendo, hapo ndipo unapoweza kuona kitu kinachoitwa ‘malavidavi’ au kwa swaga za mapenzi tunaita mahabati. Ikiwa ni kielelezo kuwa wahusika wa uhusiano wanakuwa kwenye kiwango kizuri sana cha kufurahia ‘kapo’ yao.
Tatizo kubwa hutokea pale ambapo wahusika kwenye uhusiano wanakuwa wanapishana mitazamo au uamuzi. Unajua kabisa hilo unalolifanya litamuudhi mwenzi wako lakini unakosa hofu, unatenda tu. Siku akisema “nakwenda” ndipo unashtuka na kudondosha machozi.
Ni kama unavyoelewa kuwa hakuna mtu ambaye anaweza kufurahia mwenzi wake kusaliti. Unavaa ujasiri na kuanzisha uhusiano wa pembeni. Anapobaini hilo na kuondoka zake, unapiga magoti kumzuia asichukue uamuzi huo. Akiondoka unabaki kujutia ulichomfanyia.

Itaendelea wiki ijayo.

TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

Post a Comment

Ungana Nasi, Like Page Yetu Hapa Chini