WANANCHI WAKATISHWA TAMAA NA BUNGE LA KATIBA


Wananchi kadhaa wameeleza kusikitishwa na mwenendo wa Bunge Maalumu la Katiba, huku wakimtaka Rais Jakaya Kikwete aikemee hali hiyo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk. Hellen-Kijo Bisimba, amesema, ni aibu kwa kinachoendelea katika bunge hilo.

“Leo (jana) niliacha kazi zangu na kujipa muda wa kuangalia shughuli ya hilo bunge na kwa kweli nimeishia kuwa dis-appointed (nimekatishwa tama) na nilichokiona, kiasi cha kuandika kwenye ukurasa wetu wa face book,” alisema.

Alisema alishangaa sana jinsi wajumbe wanavyozomeana, kiasi cha kutomsikiliza hata mwenyekiti, kinyume na utaratibu unaowataka wajumbe wakae pale mwenyekiti anaposimama.

“Mivutano yao haina tija na badala yake wanapoteza hela za Watanzania bure…yaani kama kwa kipindi chote cha wiki tatu bado wanahangaika na kanuni, itakuwaje wakiifikia rasimu yenyewe,” alisema.

Dk. Bisimba alisema ili kuwaweka kwenye msitari, ni wakati wa Rais Kikwete aliyewateua sasa kuikemea hali, ili warudi kufanya kazi iliyowapeleka ya kutupatia katiba tunayoitaka.

Profesa Mwesiga Baregu alisema hali hiyo inatokana na wajumbe kutopata semina ya kuwaandaa.

“Tungekwenda sawa kama wangepata semina ya kuwafunda ili wajue kilichowapeleka kule, na kitu gani wananchi wanakitarajia kutoka kwao, bahati mbaya haikuwepo,” alisema na kwua kinachoonekana katika kadhia hiyo, ni kutokuwepo kwa ratiba ya kuliongoza hilo bunge.

“Nasema hivyo kwa sababu ukiwa na ratiba, itakuongoza katika shughuli zako kwa kuwa utaangalia shughuli ulizo nazo na muda ulio nao, na itakusaidia kujitathmini kama unaenda vizuri,” alisema.

Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Benson  Bana, alisema mambo yanayofanyika Dodoma katika Bunge la Katiba yanawahuzunisha wananchi.

Pia, alisema bunge hilo halikufanyiwa maandalizi mazuri kabla ya kuanza na ndiyo maana mambo hayo yanatokea.

Aidha, Dk. Bana alisema Bunge hilo linayumba kwa sababu bado halijapata Mwenyekiti wa kudumu na kwamba anaamini akipatikana Mwenyekiti wa kudumu litatulia na kuendeshwa vizuri.

Aliitaka Kamati inayomshauri Mwenyekiti wa muda izingatie suala la muda kwa sababu kuahirishaahirisha kunaweza kuchelewesha kufanikisha shughuli  hiyo.

Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana, alisema wabunge wanatakiwa kufanya kazi kwa umoja na ushirikiano ili waweze kufanikisha kazi hiyo.

Alisema watanzania wanahitaji kupata Katiba nzuri, lakini wabunge wa bunge hilo wanatakiwa kuzingatia muda na kutolifanya bunge hilo kuwa mzigo mkubwa kwa kuwa gharama inayotumika ni kubwa.

“Naelewa umuhimu wa kupata muafaka, lakini ninaomba usicheleweshwe sana na ukasababisha mambo mengine yashindwe kufanyika, wakumbuke pia kwamba hapo baadae watahitaji kuingia katika bunge la bajeti,” alisema Kinana na kuongeza.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba, Deus Kibamba, alisema tatizo kubwa linalosabisha kutokea kwa vurugu katika bunge hilo ni kutokana na wajumbe kutakunguliza maslahi ya vyama vyao na kusahau kwamba kilichowapeleka ni kwa ajili ya Watanzania.
 
SOURCE: NIPASHE

TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

Post a Comment

Ungana Nasi, Like Page Yetu Hapa Chini