KAULI YA WAZIRI WA ELIMU YAWACHEFUA WALIMU


Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kimekerwa na kauli ya Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa , kuwa serikali inaendelea kujadiliana na taasisi za fedha juu ya namna ya kulipa deni la malimbikizo ya mishahara ya  walimu yanayofikia Sh. bilioni 61.

CWT  imesema kauli hiyo ya serikali ni kutafuta visingizio baada ya  kushindwa kutekeleza ahadi yake kuwa ifikapo Februari, mwaka huu deni la walimu litakuwa limelipwa.

Rais wa CWT, Gration Mkoba,  alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana.

Alisema majadiliano ya mishahara ya walimu yalitokana na mgomo wa  2012 baada ya kukaa kwenye meza ya majadiliano na serikali ilikubali kulipa deni na kuandaa utaratibu wa kupandisha walimu madaraja.

“Inasikitisha kuona majadiliano yanahusisha waandishi wa habari bila ya kujua kuwa kwa kauli yake waziri tayari  walimu wameingia kwenye mgogoro na serikali, lakini  nawasihi walimu wasubiri tamko rasmi la mgogoro,” alisema.

Mkoba alisema tangu serikali ilipoahidi kutekeleza madai yao, hakuna hata dai moja  lililotekelezwa  lakini imewashangaza kuona ikijinadi kuwa inaendelea na majadiliano ya kulipa deni hilo wakati majadiliano hayana tija kwa mwalimu.

Alisema Novemba, mwaka jana mkutano mkuu wa CWT ulitoa siku 60 kwa serikali kukamilisha taratibu zote la kulipa malimbikizo ya mishahara ya walimu nchini.

Pia Januari mwaka huu kwenye kikao cha Baraza  la Taifa la CWT kiliazimia kuwa ifikapo mwishoni mwa Februari, mwaka huu, ikiwa serikali itashindwa kulipa malimbikizo hayo litakuwa tayari kuongoza mgomo.
 
CHANZO: NIPASHE

TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

Post a Comment

Ungana Nasi, Like Page Yetu Hapa Chini